Sunday, June 30, 2013

KIFAA CHA KUTOA TAARIFA DUNIA NZIMA CHA GUNDULIWA


Mtu yeyote anaweza kukimiliki. Ni kidogo na rahisi kubebeka. Kimetengenezwa na kampuni maarufu ya huduma za mitandao ya kompyuta ya Google ya nchini Marekani.
Kifaa hicho chaweza kuvaliwa kama miwani na kimetengenezwa kwa teknolojia inayomwezesha mmiliki kusambaza sauti na picha kwenye mitandao ya kompyuta kwa sekunde moja tu na kumfikia mtu yeyote akiwa sehemu yoyote duniani.
Ni teknolojia ambayo imekusudiwa kuanza kutumika duniani mwanzoni mwa mwaka ujao, hivyo kuleta changamoto nyingine ya mawasiliano duniani.
Hii itasaidia watu kuweza kuwasiliana kirahisi na wenzao kwa kutumia sauti na picha. Kinachofanyika ni kwamba mtu mwenye kifaa hicho anaweza kuchukua sauti na picha za matukio kwenye eneo alipo.
Picha na sauti hizo ataweza kuziingiza kwenye mtandao wa mawasiliano ya kompyuta kwenye wafuti au mitandao ya kijamii kama vile blogu, facebook na twitter, hivyo kuwafanya watu wote wanaozitembelea kuona picha na hata kusikia sauti.
Vifaa hivyo vimeambatanishwa kwenye fremu ambayo mtumiaji atavaa kama miwani. Si lazima miwani hiyo iwe na kioo, hivyo kwa wale wasiopenda kutumia miwani wanaweza kuitumia.
Kifaa hicho kinaweza kuambatanishwa na miwani ya kawaida ama ile ya kuzuia mwanga mkali. Ndiyo maana kimepewa jina Google Glass ama kwa tafsiri isiyo rasmi Miwani ya Google.
Kwa namna kinavyofanya kazi ni sawa na kompyuta ama simu hasa kutokana na kuwa na kioo cha kuona. Kina kamera na kinasa sauti na kina uwezo wa kujiunga na mawasiliano ya mtandao wa kompyuta kwa kutumia programu ya Wife ambayo hauhitaji waya kuunganishwa.
Kifaa hicho kina kioo kidogo kilichowekwa juu ya jicho moja, ambacho mtumiaji hukitumia kuangalia namna anavyojiunga kwenye mtandao wa mawasiliano.
Kioo hicho ni sawa na kile cha simu au cha kompyuta lakini ni kidogo sana ingawa kwa kuwa kipo karibu sana na jicho humfanya mtumiaji kuona kwa ukubwa namna anavyoingia kwenye mtandao wa kompyuta na kujiunga na eneo la mawasiliano alilokusudia.
Kifaa hicho kinatumia teknolojia ya kugusa ama kama ilivyozoelaka ‘touch’. Mguso huo wa kupapasa haufanyiki kwenye kioo kama ilivyo kwenye simu bali pembeni sambamba na eneo la fremu ya miwani inayojishikilia juu ya sikio.
Kwa kupapasa, mtumiaji anaweza kutembelea wavuti mbalimbali ama kutafuta sehemu yake ya mawasiliano kwa kutumia mtandao wa Google.
 Mtumiaji akiingia kwenye mtandao aliokusudia, hapa anaweza kutumia teknolojia mpya ya Google kuunganisha mawasiliano na kuanza kuingiza picha na sauti kama anavyopenda.
Teknolojia hiyo imefanyiwa majaribio kwenye maeneo mbalimbali duniani na wengi wameikubali kwa kuwa itasaidia mawasiliano ya papo kwa papo kama inavyojulikana kwa wengi, kupata matukio ‘live’.
Bei halisi ya kifaa hicho bado haijafahamika ingawa tathmini za awali zinakikadiria kuuzwa kwa wastani wa Dola za Marekani 1,500 sawa na Sh2.4 milioni.
Hofu ya matumizi
Mitandao mbalimbali ya kompyuta iliyoripoti mijadala mbalimbali sehemu ambazo Google Glass kimefanyiwa majaribio, wamekuwa na wasiwasi kwamba kinaweza kutumika katika kuingilia uhuru binafsi wa mtu pamoja na kusambaza picha za ngono.
Mmoja wa wataalamu wa kampuni ya Google aliwatoa wasiwasi akisema wataweka programu maalumu ya kusimamia mawasiliano itakayozuia usambazaji wa picha za ngono.
Faida za Google Glass
Wataalamu mbalimbali waliopata fursa ya kutumia teknolojia hiyo, walisema itakuwa na faida nyingi hasa katika uwanja wa elimu.
Kwa mfano walisema mwalimu mmoja anaweza kutumika kufundisha somo moja kwa wanafunzi waliopo sehemu mbalimbali duniani kwa gharama kidogo.
Kwa kutumia teknolojia hiyo wanafunzi wanaweza kusikia sauti na kuona kwa vitendo picha ama vielelezo anavyovitumia mwalimu katika kurahisisha uelewa.
Mmoja wa wataalamu waliofanyia majaribio teknolojia hiyo ni Dk Rafael Grossmann, ambaye aliandika kwenye mtandao wake wa kijamii kuwa itasaidia kuwafundisha wanafunzi wake hata wakati anamfanyia upasuaji mgonjwa bila wao kuwepo.
Jambo jingine la faida kwa teknolojia hii ni katika tiba. Inaelezwa kuwa kwa kutumia kifaa hiki daktari moja bingwa anaweza kuhudumia hospitali nyingi akiwa ofisini kwake.